PDA

View Full Version : Kesi za EPA: Tunachoshuhudia ni mazingaombwe?



mwanakijiji
12-04-2008, 04:47 PM
(Toka Tanzania Daima, Jumatano Disemba 3, 2008)
Na. M. M. Mwanakijiji

TUTAKUWA ni waongo na wanafiki endapo tutabeza hatua tunazozishuhudia mbele ya macho yetu leo hii na kwa hakika tutakuwa wakanao historia kama hatutakubali uhistoria wa kile kinachotokea mbele yetu.

Macho yetu yanashuhudia kitu ambacho tafsiri yake yaweza kuwa ngumu kueleweka hadi pale kitakapochambuliwa vizuri. Aidha tunashuhudia mazingaombwe ya daraja la kwanza au mbele yetu tunachoona ni ndiyo “kitu chenyewe”.

Haya ni mazingaombwe?

Kati ya vitu ambavyo vinazungumzwa sana mitaani kufuatia hatua za serikali kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wa vitendo mbalimbali vya kifisadi ni kama kweli tunachokiona ni ukweli au uzugaji tu.

Nimejiuliza kwa muda kwa nini watu hawajarukaruka kama kulungu kwa furaha kuona watuhumiwa wa ufisadi wakifikishwa mahakamani? Kwa nini kuna watu wanaona kinachoendelea ni mazingaombwe? Je tuna sababu ya kuona fahari au kujisikia kuwa tumepiga hatua kwenye vita vya ufisadi au matumizi mabaya ya madaraka? Fuatana nami.

Siyo mara ya kwanza kwa vigogo kufikishwa mahakamani.

Kuna kizazi cha Watanzania ambacho hakijawahi kushuhudia kesi nzito zinazowahusu watu waliowahi kuwa na nafasi serikalini au wale ambao kwa namna fulani wanaaminika kuwa wana ujiko wa aina fulani katika siasa za nchi yetu. Kizazi hiki bila ya shaka kinashangazwa na kutiwa moyo na hatua hizi za kufikishwa mahakamani wale wafanyabiashara ambao wanatuhumiwa wizi wa mabilioni, watumishi wa umma waliowezesha wizi huo na wale viongozi wa kisiasa ambao kutokana na nafasi zao wanadaiwa kuzembea na kulisababishia taifa hasara kubwa.

Hapa tunawategemea wataalamu wetu wa sheria na historia watatusaidia kuweka kesi hizi katika maudhui yake yanayostahili. Mwalimu Nyerere aliwahi kushtakiwa mahakamani na serikali ya kikoloni kwa makosa ambayo wakati ule yalionekana kuwa yana msingi.

Baada ya Uasi wa Kijeshi mwaka 1964 ambao ulisababisha uundwaji wa JWTZ tunavyoliona leo kulikuwa na msukosuko serikalini kitu ambacho baadaye kilisababisha mashtaka ya uhaini kuletwa katika kundi la watu ambao walikuwa ni wasaidizi wa karibu wa Nyerere na watendaji wa serikali.

Mionongoni mwao ni Oscar Kambona na Bibi Titi Mohammed. Ninawataja hao ili kuonesha kuwa kesi dhidi ya kiongozi au mtu aliyewahi kuwa kiongozi katika serikali au chama siyo ngeni nchini.

Siyo lengo langu kuangalia kesi hizo bali kuonyesha tu kuwa kama taifa tumeshawahi kuwa hapa. Kesi za kina Kambona na wenzake zilipaswa kuitikisa nchi, lakini kama taifa tuliweza kuhimili na kuendelea kuwepo.

Kesi nyingine ambayo naweza kuiweka hapa kuonyesha kuwa Tanzania imeshawahi kupitia msukosuko wa kesi kubwa na taifa likaendelea kuwepo ni kesi ya uhaini ya miaka ya themanini. Ni moja ya kesi zilizokuwa wazi na watu waliweza kuifuatilia kwa karibu sana; mwishoni mwa kesi ile kuna watu walipata kifungo na wale walioachiliwa. Pamoja na uzito wa kesi hizo mbili za uhaini, kosa kubwa zaidi dhidi ya jamhuri yetu, taifa bado lipo na limeendelea kuwepo.

Kwa upande wa biashara kuna kesi za uhujumu uchumi za miaka ya themanini. Kesi zile zilitufundisha mambo mengi sana na kutoa mafunzo makubwa juu ya utawala wa sheria.

Bahati mbaya sana baadhi ya kesi zile za uhujumu uchumi ushahidi wake ulikuwa mbovu na uendeshaji wake ulikuwa mbaya ambao baadaye ulisababisha rufaa zake kushinda na hatimaye walioshtakiwa kujikuta wakilipwa fidia kubwa kabisa. Ulimwengu wa biashara ulitikisika nchini na hofu iliwajaa watu.

Wakati ule hatukuwa na “mafisadi” tulikuwa na “Wahujumu Uchumi” watu waliotumia hali mbaya ya uchumi kuficha mali na kusababisha upungufu wa bidhaa katika jamii na kusababisha bei kupanda (bei ya kuruka). Kipindi hili biashara ya magendo ilitamalaki.

Baadhi ya mambo tunayoyafanya leo katika biashara msingi wake ni wakati wa uhujumu uchumi. Leo hii hata baadhi ya watu wanavyokwepa kodi, kuficha mali misituni, au kutumia “njia za panya” kuingiza mali nchini ni kutokana na mawazo ya “kilanguzi”. Tulikuwa huko, tukayaona na kama taifa tumesalimika.

Kwa upande wa madaraka kesi nzuri ambayo inaweza kutajwa hapa ni pamoja na kesi ya aliyekuwa Waziri wa Ujenzi, Nalaila Kiula, ambaye Serikali ya Mkapa ilimfikisha mahakamani na hatimaye baada ya mchakato akaachiwa jina lake likiwa limechafuliwa sana.

Leo hii serikali ile iliyomfikisha mahakamani imeshindwa kumpa nafasi ya kuitumikia nchi yake tena! Pamoja naye tunakumbuka alifikishwa katibu wa Wizara yake George Mlingwa ambaye alikutwa na hatia Mahakama Kuu, katumikia kifungo kwa muda hadi aliposhinda katika Mahakama ya Rufaa. Taifa liliyaona, likaendelea kuwepo.

Lakini kama kuna wakati ambapo tungeshtuka zaidi ni pale Rais Mkapa alipowastaafisha kwa manufaa ya umma maafisa wa ngazi za juu wa polisi ambao walituhumiwa kujihusisha na vitendo vya kifisadi.

Kustaafishwa kwao kulisikika radioni na wananchi wakaamini, kama si wote, kuwa ni mapambano dhidi ya ufisadi. Bahati mbaya au kutokana na uzembe wa Mwanasheria Mkuu maafisa wale hawakupiga magoti na kusalimu amri kwani baadhi yao walikuwa ni wanasheria na wote walijua haki yao kwa mujibu wa sheria ya polisi. Wakakata rufaa, wakaweza kuthibitisha katika mahakama zetu kuwa Rais hakufuata sheria kuwastaafisha na hivyo kudai mamilioni ya shilingi. Wakashinda! Taifa likaona, na likaendelea kuwepo.

Leo hii kuna kesi inaendelea ya aliyekuwa balozi wetu kule Italia ambaye anashtakiwa mfano wa makosa wanayoshtakiwa leo kina Mramba na watendaji wengine. Kesi inaendelea lakini hakuna la kushtua kwani tumewahi kufika hapa kama Taifa.

Hivyo mifano hiyo michache ya kesi kubwa kubwa ni ushahidi tosha kuwa Tanzania haiwezi kutikisika au kushangazwa kwa kushtakiwa viongozi au mtumishi wa juu wa umma. Tumeshayaona haya! Taifa letu haliwezi kushtushwa kusikia mfanyabiashara mkubwa ametinga kizimbani kwa tuhuma za ufisadi; tumeyaona hatuwezi kushtuka ati aliyekuwa waziri kafikishwa mahakamani! Hatuwezi kushtuka kusikia afisa usalama amekamatwa kwa kutumia madaraka yake vibaya, tumeyaona; hatuwezi kusikia kuna watu wamejaribu uhaini dhidi ya jamhuri yetu au kutishia usalama wa uwepo wetu kama Taifa, tumeyaona haya (mara mbili na ya tatu kule Zanzibar ilipanguliwa!).

Hapana, wananchi wasishtuke wala kutetemeshwa na haya. Tumeyaona na kwa kadiri tunavyoendelea kukua kama taifa tutayaona mengi na siku moja tusije kushangaa aliyekuwa Rais anafikishwa mahakamani au Rais aliye madarakani kaondolewa madarakani kwa mashtaka ya Bunge (impeachment). Hata hayo yote yatokee Tanzania itaendelea kuwepo!

Hivyo, kitendo cha kuwapelekea watu mahakamani peke yake hakitoshi kabisa kutufanya tuamini kuwa tunachoshuhudia siyo mazingaombwe. Niliandika karibu miaka miwili iliyopita kuelezea sanaa ya mazingaombwe ilivyo. Tutakuwa watu wa ajabu sana kama tutashangilia majigambo ya mwanamazingaombwe au mbwembwe za kuvutia onyesho.

Je ni kitu halisi?

Kuna mambo kadhaa ambayo yananitatiza kuhusu hatua hizi ambazo wengi tumelilia zichukuliwe na sasa zimeanza kuchukuliwa hatujui kama ni mazingaombwe au ndiyo “mchezo wenyewe”.

1. Mashtaka dhidi ya watuhumiwa wa EPA

Kesi yoyote ile inapoandaliwa kuna mambo kadhaa yanayoangaliwa. La kwanza na la msingi ni ushahidi uliopo na uzito wa ushahidi huo (preponderous of evidence). Ni ushahidi pekee ndio unatakiwa kuongoza msingi wa mashtaka yaliyopo lakini katika kuweza kuelewa uzito wa ushahidi huo na mashtaka gani yaletwe kinachoangaliwa ni sheria. Ni sheria ipi inayoweza kutumika kwenye ushahidi upi ili kuleta mashtaka yapi ndilo swali la msingi.

Lakini msingi wa kwanza katika mashtaka yoyote yale ni ushahidi kwani sheria zipo wakati wote mpaka pale kunapokuwepo na ushahidi wa kuvunja sheria hizo ndipo mashtaka yanapoweza kuletwa. Mwendesha mashtaka mzuri ni yule ambaye anaweza kuangalia ushahidi kwa upana wake na kuamua ni mashtaka gani ayalete dhidi ya mtuhumiwa.

Hivyo katika kesi hizi za EPA, tatizo langu la mashtaka nikisoma jinsi yalivyotolewa najikuta nahoji kama ushahidi uliopo hautoshi kuongeza mashtaka yaliyo makubwa zaidi kuliko yale ya “kula njama, kughushi, wizi na kujipatia fedha kwa udanganyifu”.

Kwa kadri mashtaka yalivyosomwa, naamini kesi hizi za EPA, haziwezi kabisa kuwa kamili bila kuongeza mashtaka ya kuhujumu uchumi (kwa mujibu wa sheria ya Kuhujumu Uchumi ya 1984) na pia mashtaka ya kufaidika kutokana na uhalifu kwa mujibu wa sheria ya “Kunufaika kutokana na Uhalifu” ya mwaka 1991. Sheria zote mbili pamoja na mabadiliko yake.

(Inaendelea Chini)

mwanakijiji
12-04-2008, 04:48 PM
Je wanaweza kushtakiwa kwa kuhujumu uchumi?

Ninaamini kuwa mashtaka dhidi ya watuhumiwa wa EPA kwa kadiri yalivyosomwa hayawezi kukamilika bila nyongeza ya mashtaka kutokana na sheria hizo mbili. Hapa tusema kuwa sheria ile ambayo wengi tunaiita ya Uhujumu Uchumi kwa Kiingereza jina lake kamili ni The Economic and Organized Crime Control Act. Sehemu mojawapo ya sheria hiyo inahusiana na mambo ya hujuma za kiuchumi (economic sabotage) lakini sehemu ya ?organized crime? mara nyingi hatujaiangalia kwa makini.

Ninaposoma mashitaka dhidi ya watuhumiwa hawa kwa jinsi walivyojipanga, na kutekeleza mipango yao, sina shaka hata kidogo kuwa walichofanya ni ?organized crime?. Tafsiri ya ?organized crime? katika sheria hiyo ni wazi kabisa inahusisha kundi la watu waliofanya kitu wakipanga kitu kama genge la kihalifu (criminal racket).

Zaidi ya yote katika makosa yanayotajwa katika sheria hiyo katika fungu la kwanza kwa mujibu hasa ibara ya 56(1), yapo makosa ambayo yanaendana bila ya shaka na madai yaliyoletwa mahakamani dhidi ya watuhumiwa.

Kutotumia ushahidi uliopo kufungua mashtaka ya kuhujumu uchumi kwa mujibu wa makosa hayo ni kuamua kumshtaki mwizi kwa kosa la wizi na kukutwa na mbuzi wakati kuna ushahidi kuwa alivunja nyumba, kuharibu mali ya watu na kusababisha hasara nyingine nyingi.

Hapa nitatumia mifano miwili tu ya haraka haraka. Ibara ya 5 ya fungu la kwanza la makosa hayo sehemu (a) inaelezea kuwa mtu atakutwa na hatia ya kuongoza genge la kihalifu endapo ?kwa makusudi na kwa kunuia anapanga, kuendesha, kuongoza, kusimamia au kufadhili genge la kihalifu?.

Je, hawa waliofikishwa mahakamani waliweza kufanya hicho wanachotuhumiwa kufanya bila kiongozi wa aina fulani? Naamini yupo mtu ambaye ameliongoza kundi hili kwani jinsi makampuni yote yanavyodaiwa kufanya katika kujipatia fedha za EPA, yamefanana sana kiasi kwamba wazo kuwa imetokea ni nasibu haiwezekani. Hivyo kuna mtu au kundi la watu ambao wamesimamia genge la kihalifu la wizi wa EPA.

Katika sehemu (b) ya fungu hilo hilo la sheria hiyo, tunaambiwa kosa jingine ambalo ni kuwa mtu atakutwa na hatia ya kuongoza kundi la uhalifu endapo ?huku anajua anawachochea au kuwafanya watu wengine watumie nguvu, ulaghai, au vitisho kutekeleza au kufanikisha malengo ya genge la kihalifu?.

Sheria hiyo endapo itaangaliwa na waendesha mashitaka wetu nina uhakika inaweza kutumiwa dhidi ya watuhumiwa hawa.

Lakini sheria nyingine ambayo nimeitaja hapo juu ambayo naamini inaweza kutumika ni ile ya ?Proceeds of Crime? ya mwaka 1991.

Sheria hiyo ina lengo la kushughulikia wote wanaonufaika na mapato au vitendo vya kihalifu au mali zinazotokana na uhalifu. Mojawapo ya mifano ya matumizi ya fedha za EPA ni uanzishwaji wa makampuni na biashara mbalimbali. Kuna wale wanaodaiwa kuanzisha nyumba za makazi au miradi mbalimbali.

Mtu mwingine anaweza kusema watuhumiwa wa EPA walitumia hela hizo ?vizuri? kwa kuanzisha makampuni mbalimbali na biashara mbalimbali. Ukweli ni kuwa kama fedha iliyotumika katika miradi yao mbalimbali imetokana na uhalifu basi sheria hiyo ingepaswa kutumika kuwaadhibu na kulazimisha kufilisi mali hizo.

Kutotumika kwake katika madai yaliyoletwa hadi hivi sasa kumeniacha na maswali. Kama wafanyabiashara hawa wote watakuja kuthibitika kuwa waliweza kufanya wanachodaiwa kufanya na ya kuwa ni kweli walijipatia fedha kwa wizi n.k hatuna budi kujiuliza walizifanyia nini fedha hizo? Yaani walinufaikaje. Na kama tayari tunajua walivyonufaika (nakumbuka tuliambiwa baadhi yao hata magari yao yalikuwa yamekamatwa) kwa nini hatuwashtaki kwa sheria hiyo pia?

Kama itaonekana kuwa fedha hizo zilitumika kununua magari, majumba, kuanzisha benki n.k basi vitu vyote ambavyo vimepatikana kutoka na fedha ya uhalifu vitu hivyo kwa mujibu wa sheria hiyo vinapaswa kutaifishwa! Kwa nini hawajashtakiwa kwa makosa ya sheria hiyo?

Lakini pia sababu nyingine ya kutumia sheria hiyo ni kufanya kile ambacho kinaweza kisifanywe nacho ni ?kufunua ushungi wa kampuni?. Mojawapo ya sababu zilizotolewa mwanzoni ni kuwa ilikuwa ni ngumu kuwashtaki watu binafsi wa makampuni haya kwa sababu makampuni ni ?watu kisheria? na jaribio la kwanza lilikuwa ni kujaribu kukwepa kuwafuata watu wenyewe na badala yake kufuata makampuni.

Tukapiga kelele vizuri na hatimaye watu walionyuma ya makampuni wameweza kufikishwa mahakamani. Hata hivyo bado kuna makampuni mengine na watu wengine na yawezekana watuhumiwa hawa wakajitetea kuwa kuwashtaki wao kama watu binafsi ni makosa. Kutumia sheria hiyo mahakama inaweza kufunua ushungi wa kampuni (lifting of corporate veil) kwa mujibu wa Ibara ya 23:1 ya sheria hiyo.

Lakini pia kutokana na jinsi fedha za EPA zilivyohamishwahamishwa kutoka Benki Kuu kwenda kwa makampuni mbalimbali na kutoka makampuni mbalimbali kwenda benki au kuzibadilisha kwa haraka kuwa bidhaa na huduma kuna uwezekano mkubwa watuhimiwa hawa wangepaswa kushtakiwa kwa makosa ya usafirishaji haramu wa fedha (money laundering).

Mwanzoni sikuweza kuona uwezekano huo kwani sheria dhidi ya Usafirishaji Haramu wa fedha ilipitishwa mwaka 2006 na hivyo kuondoa uwezekano wa mtu kushtakiwa kwa kitu ambacho hakikuwa kosa kisheria. Hata hivyo sheria hiyo ya kunufaika na uhalifu ya 1991 inagusia suala hili katika ibara ya 71:3. Kitu pekee ambacho kinaweza kikazuia mashtaka haya ni suala la muda wa kuleta mashtaka kupita kuliko kukosekana kwa ushahidi.

Kwanini hawajashtakiwa kwa makosa ya kuhujumu uchumi? Jibu lake litakushangaza na inshallah tutaliangalia wiki ijayo.

2. Jinsi watuhumiwa wanavyotendewa mahakamani:

jambo hili ni la pili ambalo linanitatiza (la kwanza ni hilo la mashtaka) kidogo limenisumbua kwani waendesha mashtaka na magereza wasipoangalia wanatengeneza mazingira mabaya ya kesi. Watuhumiwa hawa wanatuhumiwa kuiba fedha nyingi sana, hivyo ni lazima kuhakikisha kunakuwa na utaratibu mzuri wa kuwahakikishia usalama wao.

Sikupenda kuona jinsi watuhumiwa walivyoweza kutembea na kuchanganywa na watuhumiwa wengine na zaidi jinsi walivyoweza kukaa katika mahakama jinsi wanavyokaa.

Mtu mwingine anaweza kusema kwa nini wapewe upendeleo, kwangu ninachoona kuwa kama tunataka haki itendeke kweli basi ni lazima tuone haki inatendeka. Tusiwatendee zaidi ya watuhumiwa wengine kwa sababu ya chuki zetu binafsi. Hakimu asiseme kitu chochote ambacho kitachukuliwa kuwa ni kuwahukumu watuhumiwa kabla ya kuangalia ushahidi wowote, hakimu ambaye anahisia kali kuhusu mafisadi hastahili kusimamia kesi hizi.

Mahakimu ni lazima wawe watu ambao hawataangalia kitu kingine chochote, siasa zao, hisia zao au vionjo vyao isipokuwa ushahidi tu na kuufuata ushahidi huo popote utakapowapeleka. Nje ya hapo ni kufanya mchezo wa kutengeneza rufaa huko mbele.

Sikupendezwa na kitendo cha Mahakama kushindwa kuongeza muda ili kuhakiki hati za kumiliki nyuma ili kina Mramba waachiwe kwa dhamana. Kitendo cha kuwanyima dhamana kwa sababu ya ?muda wa serikali kuisha? ni kitendo cha uonevu mkubwa dhidi ya raia. Kuna watu ambao wamefurahia kuona kina Mramba na Yona wanalala keko ?weekend? kwani kuwaachia ile Ijumaa kungemuwezesha Mramba kuhudhuria ndoa ya bintiye. Mtu mwenye mawazo hayo ana dalili za kionevu.

Kina Mramba ni washtakiwa tu na hadi hivi sasa hakuna ushahidi wowote uliotolewa mahakamani kuonyesha kuwa wamefanya wanachotuhumiwa kufanya. Sasa wanapogombania haki yao ya dhamana mahakama ni lazima iwape muda wote unaohitajika kwenye sayari yetu kutimiza masharti hayo.

Na kimeniudhi hiki kisingizio cha muda kwa sababu serikali hiyo hiyo haikukumbuka muda wa kazi pale ilipokata rufaa saa tatu za usiku kusimamisha mgomo wa walimu.

Ina maana kuwa rufaa za serikali zinaweza kusikilizwa hadi saa tatu za usiku lakini za raia wa Tanzania zinaisha saa kumi za jioni!? Ina maana serikali iko juu ya sheria na raia wako chini ya sheria au kile ambacho serikali inataka inaweza kupata hata ikibidi kumtafuta jaji atakayesikiliza rufaa yao usiku?

Binafsi ningependa Jaji au Mahakama Kuu iombe radhi kwa hili na kuhakikisha kuwa mwananchi wa Tanzania ambaye ana uhakika wa kushinda rufaa yake au ambaye anahitaji kutimiza makaratasi mawili matatu anafanya hivyo ili asibakie rumande kutokana na tatizo la muda. Vinginevyo tukikubali hilo tutakuwa tunakubali uvunjaji mkubwa wa haki za raia.

Nimeshangaa kuona maafisa wa magereza wanaowasindikiza watuhumiwa wamevaa fulani za kuzuia risasi na watuhumiwa wanapelekwa mbelembele ?wakavu wakavu?. Hivi akitokea mwendawazimu mmoja na kufanya jambo fulani dhidi yao tutashangaa? Kutokana na asili ya makosa yenyewe na uzito wake kwa taifa hatuna budi kuhakikisha usalama wa watuhumiwa wote hawa kwa namna ya pekee. Ni lazima tujifunze kushughulikia kesi nzito kama hizi.

Ukiondoa hayo niliyoyasema, ukweli utabakia kuwa kesi hizi ndizo zimeanza tu na hatua hizi hazina maana kama mashtaka yanayopaswa hayatafunguliwa na kuwa taratibu mbalimbali zikachukuliwa kimzaha mzaha. Ni lazima utaratibu mzuri na unaoeleweka uwekwe ili kulinda uthabiti wa mchakato mzima wa kesi hizi.

Vinginevyo, mimi nitakuwa mtu wa mwisho kushangaa kesi hizi zikitupiliwa mbali au watuhumiwa wengi wakakutwa hawana hatia kwa kukosa ushahidi au kutokana na mambo ya kiufundi.

Kama DPP na wenzake wameziandaa kesi hizi vibaya tangu mwanzo (na hapa naweza kuandika kitabu) tunachoshuhudia basi si mchakato mzuri wa sheria bali kuturidhisha tu kuwa ?si mlitaka wafikishwe mahakamani??.

Mwisho tutajikuta tunashangilia wachezaji kuvaa jezi nzuri na kujipanga mstari; tunaweza kushangilia wachezaji kukaguliwa! Na tutakuwa watu wa ajabu kama mechi imeanza tu tunaanza kufurahia ushindi ati kwa sababu tumewafunga goli moja tu! Tuangalie mchezo mzima maana kwa kadiri mambo yalivyo, sioni mechi hii kuisha dakika 90!

Swali kwako msomaji:

Je vyombo vyetu vya habari vimewatendea haki watuhumiwa hawa au kwa jinsi mambo yanavyoandikwa inaonekana tayari wamehukumiwa? Vyombo hivyo vifanye nini ili visiharibu mchakato wa kesi hizi?